MKONO ALIPUA UFISADI KIWIRA.
Posted on
Jun 22, 2012
|
No Comments
| AELEZA MGODI ULIVYOUZWA BEI YA KUTUPA,NGELEJA NAYE AZUA MTAFARUKU BUNGENI SAKATA la ufisadi katika uuzwaji wa mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira, mkoani Mbeya limeibuka upya, safari hii ikielezwa na Mbunge wa Musoma Vijijini (CCM), Nimrod Mkono kuwa umeuzwa kwa bei ya kutupa.Mbunge huyo ambaye ni mwanasheria, amelitaka Bunge kuunda Kamati Teule kwenda kuchunguza ufisadi huo, huku akihoji sababu za Serikali kuutengea mabilioni ya shilingi wakati umekwishauzwa.
Mkono alisema kuwa, “Mgodi huo wenye thamani ya matrilioni ya shilingi, umeuzwa kwa bei ya kutupa ya dola 700,000 tu za Marekani (Sh1.1 bilioni), kwa kampuni ya Intra Energy ya Australia.” Mgodi wa Kiwira uliwahi kuzua malalamiko baada ya kumilikishwa kwa Kampuni ya ANBEN Limited, mali ya Rais Mstaafu Benjamin Mkapa na mkewe, Anna Mkapa, lakini Januari mwaka huu, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja aliieleza Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), kuwa ANBEN Limited haihusiki tena na mgodi huo. Alifafanua kuwa kampuni hiyo iliondolewa kuwa miongoni mwa wamiliki wa hisa kwa vile haikuweza kulipia hisa 200,000 ilizokuwa imechukua wakati wa usajili wa Kampuni ya Tan-Power Resources (TPR). Akichangia mjadala wa Bajeti jana, Mkono alihoji sababu za Serikali kutenga Sh40 bilioni kwa ajili ya kulipa watu wa mgodi wa Kiwira ilhali inajua kuwa mgodi huo uliuzwa kwa bei ya kutupwa tangu mwaka 2007. |

