KESI YA EPA WALIPA FIDIA KUKWEPA KIFUNGO
Posted on
Nov 26, 2012
|
No Comments

WAFANYAKAZI watatu wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Ester Komu, Iman Mwakosya na Sophia Kalika wamelipa fidia ya Sh5 milioni na kuepuka kifungo cha miaka mitatu jela.
Jopo la mahakimu watatu waliokuwa wakiisikiliza kesi ya wizi wa Sh3.8 bilioni za EPA linaloongozwa na Jaji Samuel Kalua, Jaji Beatrice Mutungi na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Kisutu, Ilvin Mugeta, katika hukumu yao waliyoisoma juzi waliwahukumu wafanyakazi hao kifungo cha miaka mitatu jela ama kulipa fidia ya Sh5 milioni.
Baada ya kumalizika kusomwa kwa hukumu hiyo, Ester Komu alifanikiwa kulipa fidia ya Sh5 milioni na kuachiwa huru wakati wenzake Iman na Kalika walipelekwa gereza la Segerea hadi jana walipokamilisha maamuzi ya hukumu hiyo kwa kulipa Sh5 milioni na kuachiwa huru.
Mbali na watuhumiwa hao, wengine waliohukumiwa
katika hukumu hiyo iliyosomwa juzi na Hakimu Mugeta ni Kada wa Chama
cha Mapinduzi (CCM), Rajabu Maranda ambaye alihukumiwa kifungo cha
miaka miwili jela na kuamuriwa kurejesha Sh616.4 milioni.
Binamu yake Farijala Hussein naye alihukumiwa kifungo cha miaka mitatu jela na kuamriwa kurejesha Sh81 milioni na mfanyabiashara Ajay Soman akihukumiwa kifungo cha miaka miwili jela sawa na Maranda lakini yeye akiamriwa arejeshe Sh400 milioni.
Kabla ya kusoma hukumu hiyo iliyochukua zaidi ya saa 4, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Kisutu, Ilvin Mugeta alisema washtakiwa wote wamepatikana na hatia katika makosa ya kughushi, kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu, kuwasilisha nyaraka za uongo BoT na kuisababishia Serikali hasara ya Sh3.8 bilioni.
Hakimu Mugeta alisema wafanyakazi wa BoT
hawatahusika katika mpango wa kurejesha fedha kwa sababu ushahidi
unaonyesha hawakunufaika na chochote katika wizi huo.
Alisema Maranda, Farijala na Soman wana ushahidi
ambao unaonyesha kuwa walijinufaisha na fedha hizo hivyo wanatakiwa
kuzirejesha na kwamba iwapo watashindwa kutekeleza amri hiyo, mali zao
zikamatwe.
Wakili wa Serikali, Shedrack Kimaro awali aliiambia mahakama kuwa Maranda na Farijala walikwisha tiwa hatiani kwa makosa ya aina hiyo katika kesi namba 1161/2008 na 1163/2008 na kwamba hawana kumbukumbu ya kutenda makosa ya uhalifu kwa washtakiwa Ajay, Iman, Ester na Sophia.
Kimaro alisema kutokana na aina ya makosa na fedha za umma aliomba mahakama itoe adhabu kali ili iwe fundisho kwa wahalifu wengine wenye tabia kama hiyo.
Pia aliiomba mahakama itumie mamlaka yake iliyopo katika kifungu cha 348 (1) ama cha 358 (1) cha sheria ya mwenendo wa mashauri ya jinai sura ya 20, kuwaamuru washtakiwa hao kurejesha fedha wanazodaiwa kuiba BoT kama walivyojipatia.
Pia aliiomba mahakama itumie mamlaka yake iliyopo katika kifungu cha 348 (1) ama cha 358 (1) cha sheria ya mwenendo wa mashauri ya jinai sura ya 20, kuwaamuru washtakiwa hao kurejesha fedha wanazodaiwa kuiba BoT kama walivyojipatia.
Magafu akijibu hoja hizo, alidai kuwa
Maranda na Farijala wasipewe adhabu kali kwa sababu kesi hizo
zilifunguliwa wakati mmoja na kwamba tofauti ilikuwa ni majina ya kampuni na kuwa aliyestahili kupewa onyo kama hilo ni yule aliyefanya uhalifu na akarudia tena.
Maranda na binamu yake Farijala Hussein tayari wanatumikia kifungo cha miaka mitano jela baada ya kupatikana na hatia ya wizi wa Sh1.8 bilioni za Akaunti ya Madeni ya Nje (Epa) iliyopo BoT na kuamuriwa kurejesha kiasi hicho cha fedha.
Licha ya kutumikia kifungo hicho, pia wanatumikia kifungo
kingine cha miaka mitatu jela baada ya kupatikana na hatia katika kesi
ya tuhuma za kuchota Sh2.2 bilioni za EPA.
Hukumu hiyo ya tuhuma za wizi wa Sh3.8 bilioni za
Epa, ilisomwa na jopo la mahakimu watatu lililoongozwa na Jaji Samuel
Kalua, Jaji Beatrice Mutungi na Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Kisutu,
Ilvin Mugeta.
Katika kesi hiyo, washtakiwa hao kwa pamoja
wanadaiwa kuwa kati ya Januari 18 na Novemba 3,2005, kinyume na kifungu
namba 384 cha kanuni ya adhabu sura ya 16 ya sheria, walikula njama ya
wizi wa fedha kutoka BoT.
Pia wanadaiwa kughushi hati ya usajili yenye namba
46218 na kuonyesha kuwa zimesainiwa na kutolewa na Msajili wa Biashara
kwa Kampuni ya Mibale Farm wakati si kweli.
Wanaendelea kudaiwa kujipatia Sh3.8 bilioni baada ya kudanganya kuwa kampuni yao ya Mibale Farm imepewa deni na Kampuni ya Textile Mills Ltd ya nchini India.
Wanaendelea kudaiwa kujipatia Sh3.8 bilioni baada ya kudanganya kuwa kampuni yao ya Mibale Farm imepewa deni na Kampuni ya Textile Mills Ltd ya nchini India.