photo NAAZ_zpsd0bbd510copy_zps37715af5.jpg
 photo NAAZ_zpsd0bbd510.jpg
Nafasi Ya Matangazo
> > MEMBE AJIPANGA 'KUWATWANGA WAANDISHI VIONGOZI WANAOMCHAFUA

MEMBE AJIPANGA 'KUWATWANGA WAANDISHI VIONGOZI WANAOMCHAFUA

Posted on Jul 19, 2012 | No Comments

Waziri wa Mambo ya Nje ya Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe amefunguka na kuuelezea umma kwamba anajiandaa 'kuwatwanga' waandishi wawili na viongozi wengine tisa.
Membe al
isema kuwa amejiweka sawa kuwatwanga watu hao kwa kuwa wanamzulia mambaya na kumchafua kwa umma, kisa wanadhani ni tishio kwao na makundi yao, ikiwa ataamua kugombea urais wa Tanzania.
Mbali na tishio la kuwatwanga watu hao, Membe wakati akihojiwa na ITV katika Kipindi cha Dakika 45, pia alizungumzia masuala kadhaa yanayomkabili yeye binafsi, wizara anayoiongoza na hofu ya kuwepo ufisadi wizarani
Pia aligusia upotevu wa Sh bilioni tatu katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
Akizungumzia fedha hizo, Membe alisema baada ya Serikali ya Libya kuikopesha Serikali ya Tanzania kiasi hicho cha fedha, baadaye Serikali za nchi hizo mbili zilikutana na kukubaliana fedha hizo zikopeshwe kwa kampuni yoyote itakayozihitaji.
“Baadaye Serikali ya Libya na Tanzania zilikutana na kukubaliana fedha hizo zikopeshwe kwa kampuni yoyote itakayotaka kukopa izikope na makubaliano haya yako kwenye maandishi. Baadaye ikaja kampuni moja ya Meize kwa ajili ya kujenga kiwanda cha saruji kule Lindi na wakati wa kampeni tukawaahidi wananchi wa Lindi kwamba kiwanda hicho kitajengwa. Wakati tunaahidi hivyo, kumbe Kampuni ya Mohamed Enterprises ilikuwa inashirikiana na ofisa mmoja wa ubalozi wa Libya apate fedha hizo na hapo ukawa ugomvi.
“Pamoja na hayo, mimi nilisimamia kuhakikisha kiwanda hicho cha saruji kinajengwa Lindi kama sehemu ya kumbukumbu yangu. Lakini baadaye wananume wakabadilisha lugha, wakasema nimewapa marafiki zangu, jamani fedha hizi ni makubalino ya nchi mbili na mimi ni ‘share holder’.
“Sasa nakwambia fedha hizi ziko TIB, nendeni kwa meneja wa TIB mumuulize, huu ujinga gani huu unaozungumzwa, kwanza hata hizo Dola milioni 20 hazitoshi kujenga kiwanda bali zinatakiwa Dola milioni 60.
“Sasa nataka niwaambie wananchi wa Lindi kwamba kiwanda cha saruji kitajengwa Lindi, hivi vituko vinavyotokea nitavigonga vyote na ipo siku nitawaanika wote, lazima watu hao wajue kwamba ukikaa juu ya nyoka, ipo siku atakugonga tu. Hili nawaachia Watanzania waamue lakini kuna watu 11 wakiwamo waandishi wawili wa habari, nitawatwanga kweupe, nyie suala la urais 2015 subirini tu nitawaanika peupe bungeni tena kwa majina,” alisema Waziri Membe.

Suala la urais 2015


Alipoulizwa kama atagombea urais mwaka 2015, alishindwa kuweka wazi msimamo wake kwa kile alichosema kuwa hajaoteshwa juu ya nafasi hiyo.

“Ole wao nioteshwe, ipo siku nitaoteshwa, najua nchi hii ina watu wanaoivuruga na hawataki kuona mafanikio, ukisema unataka kujivua gamba utaona wana uwezo wa kuchonga uongo, hao wanatumia vyombo vya habari kuchonga uongo. “Kwa mfano, unawakaribisha vijana kama wa Chadema nyumbani kwako unawapa chakula baadaye wanageuza mambo, we waache tu.

“Siku moja nitawatoa kwenye magazeti kila mmoja dozi yake, nitakuja kuwatandika kila mmoja na kinachoniudhi ni kwamba hao watu wako ‘smart’ wana fedha na wanataka kutawala hata kama hawana madaraka. Ukiona mtu anaanza kudharau wakati hana madaraka, ujue hapo kuna tatizo. “Jambo jingine ni kwamba ukianza kuona katika jamii kila tatizo inalaumiwa Serikali, ujue kuna tatizo, ujue hapa kazi ipo.

Uchaguzi ndani ya CCM


Kuhusu uchaguzi unaoendelea ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), alisema chama hicho kina nafasi ya kujiimarisha kupitia uchaguzi huo. Alisema ana hamu ya kufika mwaka 2015 ashuhudie uchaguzi mkuu utakavyokuwa.

“Nina hamu ya kufika mwaka 2015 nione akina nani watarudi maana kuna wabunge wengine ni mahodari wa kuzungumza bungeni lakini majimboni hawaendi. “Utakuta mbunge mwingine anasema haungi mkono bajeti, lakini baada ya siku mbili anamuomba Waziri aliyepinga bajeti yake kwamba naomba fedha za kupeleka jimboni kwangu. “Upinzani siyo kukataa bajeti, huwezi kukataa bajeti yangu halafu kesho unakuja kuniomba fedha upeleke jimboni kwako,” alisema.

Alitaka Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni naye awe anaulizwa maswali ya papo kwa papo kupima uwezo wake katika utendaji.

Maoni ya wabunge

Wakizungumza juu ya kauli za waziri huyo, baadhi ya wabunge wameonyesha kutoridhishwa kutokana na nafasi aliyonayo katika Serikali.

Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina (CCM), alisema kitendo cha Membe kusema kuna watu 11 wanaiyumbisha Serikali, hakitakiwi kufumbiwa macho kwa kuwa kinagusa mamilioni ya Watanzania, “Huyu Membe aache maneno, hivi majuzi alisema kuna watu anawafahamu wanahusika na mauzo ya rada, sasa anakuja na suala jingine la watu 11 wanaoyumbisha nchi. “Kama kweli anawajua kwa nini asiwataje, yaani wananchi wanataabika halafu yeye anatwambia atawataja, mimi simuelewi, mwambieni awataje,” alisema Mpina.

Mbunge wa Nyamagana, Ezekiah Wenje (CHADEMA), alisema Membe anatafuta umaarufu wa siasa kwa kuwa ana kitu anachokitaka, “Huyu tumemzoea, alisema hivi karibuni kwamba anawajua wahusika wa rushwa ya rada na hadi sasa hawajawataja, sasa unafikiri anataka nini. “Kama kweli hao watu wapo kwa nini asiwataje, atutajie majina, lakini kama anadhani kuna watu kama akina Lowassa wanataka kumkwamisha asigombee urais mwaka 2015, anajidanganya kwa sababu yeye hawezi kupambana na Lowassa, huyo ni mtu mdogo kwa Lowassa,” alisema Wenje.

Naye Mbunge wa Kinondoni, Idd Azzan (CCM), alionyesha kutoridhishwa na kauli ya Membe na kusema kuwa hakumuelewa baada ya kutotaja majina ya watu hao 11.

“Mimi nilimuona akizingumza na nilipomsikia hivyo, nikashindwa kumuelewa kwa sababu kama alichokuwa akikisema hakiendani na madaraka yake. “Sasa kama kweli anawajua watu hao 11 kwa nini asiwataje, atutajie kuwafanya wananchi waendelee kuiamini Serikali yao,” alisema Azzan.

Chanzo: Magazeti ya Tanzania

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru