UHABA WA MAJI WACHANGIA KUDUMAZA KIWANGO CHA ELIMU SEKONDARI YA MALULA WILAYANI ARUMERU.
Posted on
Oct 8, 2012
|
No Comments
Uongozi
wa shule ya sekondari ya Malula iliyopo King”ori wilayani Arumeru
Mashariki mkoani Arusha umeiangukia serikali na kuiomba itatue tatizo la
kero ya maji inayowakabili shuleni hapo kwa madai kwamba linachangia
kudumaza kiwango cha elimu shuleni hapo.
Hatahivyo,
uongozi huo umesisitiza ya kwamba wanafunzi wa shule hiyo wanalazimika
kutembea umbali mrefu kusaka huduma hiyo na kujikuta wakipoteza muda
mwingi wa masomo.
Akizungumza
katika mahafali ya kwanza shuleni hapo yaliyofanyika mwishoni mwa wiki
iliyopita mkuu wa shule hiyo Rehema Mroso amesema kwamba shule yake
imekuwa ikikabiliwa na tatizo kuu la uhaba wa maji tangu ianzishwe huku
akiiomba serikali iwajengee matanki ya kuhifadhi maji kuokoa tatizo
hilo.
Mroso
amesema kwamba baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo wanalazimika kutembea
umbali mrefu wa zaidi ya kolomita 5 kusaka maji kitendo ambacho
kimechangia kudumaza kiwango chao cha elimu kwa kuwa wanatumia muda
mwingi kusaka maji.
Amesema
kwamba tatizo la uhaba wa maji limechangia kuharibu mazingira shuleni
hapo kwa kuwa hukosa maji ya kuboreshea mazingira sanjari na kusafishia
vyoo mbalimbali shuleni hapo.
Hatahivyo
amesisitiza kwamba wamekuwa wakikabiliwa na kero za uhaba wa jengo la
utawala, maabara, uhaba wa nyumba za walimu sanjari na tatizo la uzio wa
shule hali ambayo inahatarisha usalama wa wanafunzi hususani wa kike
wanaolala shuleni hapo.
Awali
akizungumza katika mahafali hayo mgeni ramsi ambaye ni Katibu Tawala wa
mkoa wa Arusha Exauds Mwanga, amesema kwamba serikali imepokea na
italifanyia kazi tatizo la kero ya maji lakini amewashauri kupanda miti
ya kutosha kwa lengo la kuhifadhi mazingira shuleni hapo.
Aidha
Mwanga ameikemea tabia ya baadhi ya wanafunzi hususani wa kiume shuleni
hapo kuvaa suruali zao chini ya makalio maarufu kama “mlegezo” huku
akisisitiza ya kwamba uvaaji huo ni marufuku hapa nchini.