MAHAKAMA YA ICTR YAHAMISHA KESI YA LUTENI KANALI MUNYARUGARAMA
Posted on
Jun 28, 2012
|
No Comments
Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda(ICTR) imekubali maombi ya mwendesha mashitaka wa mahakama hiyo ya kuhamisha kesi ya mtuhumiwa ambaye bado anasakwa na afisa wa zamani wa jeshi la Rwanda,Luteni Kanali Pheneas Munyarugarama.
Hii ni kesi ya nane na ya mwisho toka ICTR kuhamishiwa nchini Rwanda kwenda kusikilizwa katika mahakama za nchi hiyo.‘’Mahakama inaamuru kesi hii kupelekwa katika mamlaka ya Jamhuri ya Rwanda ili mamlaka hiyo iweze kupeleka kesi hiyo mara moja mbele ya Mahakama Kuu ya Rwanda kwa ajili ya kusikilizwa kwa haraka,’’ sehemu ya uamuzi huo inasomeka.Katika uamuzi wake, Mahakama iliyokuwa inaongozwa na Jaji Vagn Joensen imemwamuru mwendesha mashitaka wa ICTR kumkabidhi Mwendesha Mashitaka Mkuu wa Rwanda, nyaraka zote zinazounga mkono mashitaka dhidi ya mtuhumiwa mapema iwazekanavyo.
Amri hiyo inatakiwa kutekelezwa katika kipindi kisichozidi siku 30 tangu kutolewa kwa amri ya mwisho ya kuhamishwa kwa kesi hiyo.
Mahakama ilielezea matumaini yake kwamba ‘’Jamhuri ya Rwanda, kwa kukubali kesi toka ICTR, itatekeleza kwa vitendo ahadi iliyotoa juu ya kuzishughulikia kesi hizo kwa nia njema, uwezo ilionao na utayari wa kuzingatia viwango vya juu vya kimataiafa vya utendaji haki.’’
Luteni Kanali huyo anashitakiwa kwa makosa ya mauaji ya kimbari, kula njama za kufanya mauaji hayo, uchochezi na uhalifu dhidi ya binadamu kwa kuua, kuteketeza kizazi, ubakaji na utesaji.
Munyarugarama alikuwa Kamanda wa kambi ya jeshi ya Gako katika wilaya ya Kanzenze,eneo la Bugesera, katika mkoa wa Kigali Vijijini kati ya mapema 1993 na Mei 1994.
Alizaliwa Januari mosi, 1948 katika wilaya ya Kidaho mkoani Ruhengeri, Kaskazini mwa Rwanda.
Kesi nyingine zilizohamishiwa tayari nchini Rwanda zinahusu watuhumiwa wawili wa ICTR, mchungaji Jean Uwinkindi na kiongozi wa wanamgambo wa Interahamwe Bernard Munyagishari, watuhumiwa watano ambao bado wanasakwa, wakiwemo mameya watatu, Charles Sikubwabo, Ladislas Ntaganzwa na Aloys Ndimbati, Inspekta wa zamani wa polisi, Fulgence Kayishema na meneja mmoja wa mgahawa, Charles Ryandikayo.
source: fullshangwe blog.

